Na VENANCE JOHN
Rais wa Korea Kusini aliyeondolewa madarakani Yoon Suk Yeol ameshtakiwa kwa uasi baada ya kujaribu kutangaza sheria ya kijeshi mwezi Disemba. Jaribio lake la kutaka kulazimisha utawala wa kijeshi liliiingiza nchi hiyo katika mzozo wa kisiasa ambao haujawahi kushuhudiwa na anakuwa rais wa kwanza katika historia ya Korea Kusini kushtakiwa kwa uhalifu.
![](https://static.wixstatic.com/media/57c8da_32c76867ea974f248485924dd30a0fa4~mv2.jpeg/v1/fill/w_980,h_980,al_c,q_85,usm_0.66_1.00_0.01,enc_avif,quality_auto/57c8da_32c76867ea974f248485924dd30a0fa4~mv2.jpeg)
Shtaka hilo linakuja baada ya mahakama mjini Seoul kukataa ombi la kuongeza muda wa kuzuiliwa kwa Yoon, jambo ambalo lilimaanisha kuwa waendesha mashtaka walipaswa kufanya uamuzi wa kumfungulia mashtaka au kumwachilia huru kabla ya leo Jumatatu. Timu ya wanasheria ya Yoon ilikosoa shitaka hilo na kuahidi kufichua ukiukaji wowote katika uchunguzi.
Nchini Korea Kusini, uasi unaadhibiwa kwa kifungo cha maisha jela au kifo. Hata hivyo nchi hiyo haijatekeleza mauaji katika miongo kadhaa. Pia mahakama ya Kikatiba imeanza kujadili iwapo itamfukuza rasmi Yoon kama rais au kumrejesha kazini.
Rais aliyetimuliwa amekataa kwa kiasi kikubwa kushirikiana na wachunguzi wa jinai juu ya tamko la sheria ya kijeshi. Yoon anatarajiwa kufikishwa mahakamani pamoja na waziri wake wa zamani wa ulinzi na makamanda wakuu wa kijeshi, ambao wanatuhumiwa kumsaidia kupanga na kutekeleza jaribio la kunyakua mamlaka kamili.
Comments