Na VENANCE JOHN
Baada ya kiongozi wa kiroho wa madhehebu ya Shia na Ismailia wa dini ya Kiislamu Aga Khan kufariki, sasa Prince Rahim Al-Hussaini ametangazwa kuwa Aga Khan mpya. Atachukua nafasi hiyo kutoka kwa baba yake Prince Karim Aga Khan, aliyefariki Jumanne akiwa na umri wa miaka 88.
![](https://static.wixstatic.com/media/57c8da_de8c1ce5fd2d4892b2bb5414b5fddf42~mv2.jpeg/v1/fill/w_980,h_980,al_c,q_85,usm_0.66_1.00_0.01,enc_avif,quality_auto/57c8da_de8c1ce5fd2d4892b2bb5414b5fddf42~mv2.jpeg)
Taarifa ya Mtandao wa Maendeleo wa Aga Khan imesema uteuzi huo ulifanywa baada ya wasia wa Prince Karim kuwekwa wazi. Prince Rahim Al-Hussaini Aga Khan V atakuwa Imamu wa 50 wa Waislamu wa Ismailia, ambao wanasema wao ni kizazi cha moja kwa moja cha Mtume Muhammad.
Ismaili ni madhehebu ya Waislamu wa Shia ambao ni wafuasi wa Maimamu kadhaa, akiwemo Imam Ismail, aliyefariki mwaka 765 baada ya kuzaliwa Yesu (AD). Idadi yao duniani kote inafika milioni 15, wapatao 500,000 wakiwa nchini Pakistani. Pia kuna idadi kubwa ya wafuasi nchini India, Afghanistan na sehemu za Afrika.
Prince Karim Aga Khan alimrithi babu yake kama Imamu wa Waislamu wa Ismailia mwaka 1957 akiwa na umri wa miaka 20. Prince Rahim ana watoto wawili wa kiume kupitia ndoa yake na mwanamitindo wa zamani wa Marekani Kendra Spears.
Comments